Jumatatu, 1 Julai 2013

Bomoa ya Obama ina bima?


Kwa ufupi
  • Na katika wiki hii moja iliyopita, Makengeza, naona hii misimamo mitatu imesimama zaidi na zaidi. Ni dhahiri kwamba sipendi kabisa kuona uharibifu wa aina yoyote ile.


Jamani nchi yetu! Si salama na watu wakienda huko usalama unahama kabisa. Ndiyo maana sishangai kupata barua lukuki kutoka huko. Nimechagua moja tu.
 Makengeza,
Nimeona mengi katika maisha yangu ndiyo maana siamini mengi. Lakini kuna mawili ambayo yanajidhihirisha kila wakati.
1. Mtu akipotosha ukweli makusudi, ujue maslahi yake yamo humu.
2. Mtu akihemka kupita kiasi ujue maslahi yake yameguswa pia.
Huko ninakokaa kijijini, kuna jirani mmoja ambaye ni mhamiaji. Anawadharau wenyeji hakuna mfano. Anawatukana eti ni wavivu, wajinga, hawana mawazo ya maendeleo, angekuwa na uwezo angewafutilia mbali. Kumbe shida yake ni kwamba anataka kuweka bomba yake mwenyewe kwenye chemchemu ya kijiji ili avute maji anavyopenda na wanamzuia wakisema kwamba chemchemu kile ni kwa faida ya wenyeji wote pale.
Huyu jirani anaona kwamba kwa kuwa ana pesa zisizohesabika, ana haki ya kufanya apendavyo bila kuwajali wenyeji wa eneo hili. Na anapoenda kwa wanene wenzie daima kazi yake ni kuwakashifu viongozi wa kijiji eti wanaharibu vyanzo vya maji, wana ubaguzi dhidi ya wahamiaji na kadhalika. Kumbe yeye ndiye mwenye ubaguzi na yeye ndiye anayetaka kuharibu vyanzo.
Naam na hapo nakumbuka imani yangu ya tatu ya maisha.
3.Ukiona mtu anamshutumu mwenzie kwamba ana tabia fulani mbaya, bila shaka mshutumu yumo humohumo.
Kweli kabisa. Kwa nini atuhumu mwenzie anatembea nje bila ushahidi wowote kama na yeye hana tabia ileile?
Na katika wiki hii moja iliyopita, Makengeza, naona hii misimamo mitatu imesimama zaidi na zaidi. Ni dhahiri kwamba sipendi kabisa kuona uharibifu wa aina yoyote ile. Sipendi kuwaona watu ambao huenda hawana hatia wanatiwa hasara katika maisha yao, iwe ni kwamba wamepokonywa ardhi au mali yao na wanene wasio na huruma, iwe ni kwamba wameharibu mali ya wenzao katika kumaliza hasira ya kupokonywa au kudanganywa.
Inabidi niseme hivyo maana wanene wanapenda majibu mepesimepesi kwenye masuala mazito. Kama yule aliyekuwa mdola wa Dar es Salaam, ambaye alijaribu kumnyamazisha mtu yeyote anayejaribu kueleza hali halisi ya wauza ngono eti ni wateja wao. Hii tabia ya kutoa kashfa badala ya hoja inakera sana. Na hata katika hali hii ya sasa ukijaribu kufunua pazia ili watu waone sawasawa, waambiwa na wewe mchochezi.


Tena hili neno mchochezi limetiwa mbolea hadi limesambaa kama magugumaji. Hapa kijijini kwangu, ukiulizia mapato na matumizi huko kijijini, unaitwa mchochezi, ukitaka kujua kwa nini mwenyekiti wa kijiji ameporomosha bonge la hekalu huku shule ya ukata inazidi kukatika licha ya michango ya wananchi, ni mpinzani, ni mchochezi. Ukihoji kwa nini mwekezaji hawekezi bali anapora laivu, mchochezi. Na sasa ukisema wananchi wa mahali fulani wana hoja, mchochezi pia. Funika hoja kwa kuwakashifu wenye hoja.
Lakini hebu tuache kutafakari kifukara. Hata kama wako wachache wanaopiga kelele eti gesi haitoki Mtwara ngo! Hili si dai la wanaMtwara walio wengi. Wanajua hawawezi kula gesi au kulimia gesi au kunywea gesi. Wana akili zao licha ya kashfa zote. Wao wanataka kufaidi rasilimali iliyopo kwenye eneo lao. Sasa hapo kuna mambo mawili. Si kweli kwamba wengine hawadai hivyo. Wanaoishi kandokando ya mbuga za wanyama wanapaswa kulipwa kiasi fulani (hata kama haitoshi).
Wanaoishi karibu na migodi mikubwa wanadai kuboreshewa miundombinu na huduma za jamii (hata kama haitoshi). Wanaolima mazao mbalimbali wanataka mazao yao, kama pamba kwa mfano au kahawa, yashughulikiwe palepale. Kwani kiwanda cha kahawa kiko Dodoma? Vinu vya pamba viko Mtwara? Kwa hiyo dai lao ni sawasawa na madai ya watu kila mahali Tanzania. Wafaidi wao kwanza siyo badala ya wananchi.
Pili, wana ugonjwa unaoitwa katika ung’eng’e ahadiosis … yaani uahadizi. Wamesikia ahadi nyingi kiasi kwamba ahadi zinawadhuru maana wamekata tamaa na hizi ahadi. Ni ugonjwa mbaya maana huleta homa ya ubongo, huchemsha bongo hadi washtuka wameingia mitaani katika kujaribu kutuliza jinsi ubongo unavyochemka.
Ndiyo maana wakiona mipango inaendelea kama awali huku ahadi zinamwagwa wanaona kwamba wanadanganywa. Na siyo wao tu. Wafugaji sehemu nyingine ni vivyohivyo na wachimbaji wadogo sehemu mbalimbali vilevile. Wanaona mifano lukuki kila siku. Kwani haya mashangingi yote yanatokana na nini?
Tatu, wanene wanapodai kwamba maliasili ni mali ya Wabongo wote, wanasema kweli? Kwelikweli. Ni mali ya mwanakijiji wa Tanganyika huko au ni mali ya wanene wenyewe tu? Hii siyo sababu kwa nini wamehemka hadi wanatoa povu? Wanaona kwamba wana asili ya mali, ndiyo maana rasilimali ya wote kiasili ni wao. Ndipo hapo niliposema ukiona mtu anamshtumu mwenzie tabia fulani, ujue anayo yeye.
Nne, Waswahili wamesema siku nyingi. Afichaye ugonjwa, mauti humfichua. Wale waliopewa jukumu la kulinda amani ndani ya nchi wamefichiwa magonjwa yao miaka nenda rudi. Hebu angalia tafiti. Nani ana imani nao. Nani anaamini kwamba akienda kutoa taarifa kwao hatatolewa upepo bila hata kushughulikiwa? Nani haongelei suala la rushwa miongoni mwao? Hii ni hatari sana. Maana kwa imani yangu huwezi kulinda usafi wa eneo kama wewe mwenyewe ni mchafu. Na iwapo umeshadharaulika kutokana na uchafu wako, hautasikilizwa, wala kuheshimiwa. Lakini wameachiwa kuendelea kujichafua hadi basi. Kwa hiyo, badala ya kutumia jeshi letu kulinda nchi dhidi ya maadui wa nje tunawatumia dhidi ya raia wenzetu. Hatari kwelikweli.
Lakini zaidi ya yote, watu wakilipuka kwa wingi, huwezi kudhibiti hali kwa mkong’oto. Ni hesabu rahisi sana. Ukimkung’uta mmoja, umeshachokoza wenzake wanne ambao hawapendi kuona uonevu huo. Kwa hiyo wanaamka na wao inabidi kuwakong’ota wote hao wanne. Na wao pia wana wanne wao watakaokasirika pia yaani watu kumi na sita. Wakikong’otwa na wao, ni watu sitini na nne … baada ya hapo mia mbili hamsini na sita, kisha 1024, kisha 4096 …. na kadhalika. Huwezi kuyafunika maji yakianza kububujika. Hivi, Msumbiji Kaskazini wana gesi kuliko sisi? Mbona hatusikii fujo za namna hiyo?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni