Jumapili, 18 Agosti 2013

Wataalamu wa silaha za kemikali wawasili Syria


Timu ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa wa silaha za kemikali imewasili mjini Damascus Syria leo ili kuchunguza kama silaha hizo hatari zimetumika katika vita vya ndani nchini humo au la. Serikali ya Rais Bashr al- Assad imesema makundi ya kigaidi yanayoungwa mkono na madola ya kigeni yametumia silaha hizo dhidi ya raia huku Marekani ikiielekezea serikali ya Damascus kidole cha tuhuma kuwa ndiyo iliyotumia silaha hizo. Kama ulivyo mgogoro wenyewe wa Syria kadhia ya utumiaji silaha za kemikali nayo pia imeyagawa madola makuu ya dunia. Wakati Russia inasisitiza kwamba waasi walitumia gesi aina ya sarin katika mji wa Aleppo mnamo mwezi Machi mwaka huu, Marekani inadai kwamba vikosi vya serikali ya Syria vilitumia japokuwa ni kwa kiwango kidogo silaha za kemikali dhidi ya waasi.
Timu hiyo ya wataalamu 20 wa Umoja wa Mataifa inayojumuisha wataalamu kutoka Shirika Linalopiga Marufuku Silaha za Kemikali (OPCW) inaongozwa na mwanasayansi kutoka Sweden Ake Sellstrom. Kwa mujibu wa timu hiyo, watakachofanya ni kujaribu kubaini kama silaha za kemikali ikiwemo sarin na gesi nyengine za sumu zimetumika katika vita vya Syria na si kutaka kujua ni nani aliyetumia silaha hizo. Wataalamu hao wa silaha za kemikali watafanya uchunguzi katika eneo la Khan al- Assal na sehemu nyengine mbili ambazo bado hawajaziainisha…

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni