Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam
Tanzania, limeviruhusu vyama vya Chadema, CUF na NCCR Mageuzi kufanya
mkutano wao wa hadhara kwenye viwanja vya Jangwani hapo kesho Jumamosi,
Septemba 21, lakini limewazuia wafuasi wa vyama hivyo kufanya
maandamano. Awali vyama hivyo vilikuwa vimeitisha maandamano hayo ambayo
yangewashirikisha viongozi, wanachama na wafuasi wa vyama hivyo kwa
kuanzia eneo la Tazara hadi viwanja vya Jangwani jijini Dar es Salaam,
lakini Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es salaam, Kamishna Suleiman Kova
amekataa suala la kufanyika maandamano hayo kwa madai kuwa, yanaweza
kuzusha machafuko. Lengo la kuitishwa maandamano na mkutano huo
ni kupinga mchakato mzima wa Katiba mpya na kumshinikiza Rais Jakaya
Mrisho Kikwete asiusaini Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko
ya Katiba kwa kuwa umehodhiwa na Chama Cha Mapindizi CCM. Kwa upande
mwingine Kova amesema kuwa, Jeshi la Polisi limepata taarifa za kijasusi
kuwa, vyama hivyo vimeandaa uhamasishaji mkubwa kwa watakaotumia
pikipiki na watembea kwa miguu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni