Jumapili, 28 Julai 2013

Marekani yasikitishwa na mauwaji ya Misri

Marekani imetaka mataifa ya Kiarabu kufanya jitihada za kuiondoa haraka Misri katika machafuko baada ya vikosi vya usalama kuuwa idadi kubwa ya wafuasi wa rais aliyeondolewa madarakani, Mohamed Mursi na kufungua ukurasa mpya wa hatari kati ya jeshi kukabiliana na wafuasi wa chama cha Udugu wa Kiislamu. Maelfu ya wafuasi wa chama hicho wamekesha katika msikiti mmoja mjini Cairo kuamkia leo hii kwa lengo la kutetea haki yao pamoja na serikali kutishia kuwasambaratisha mara moja. Tukio la umwagikaji damu la jana, lililotokana na maandamano makubwa, limelitumbukiza taifa hilo la Kiarabu lenye idadi kubwa ya watu katika mgogoro mkubwa baada ya kadhia ya kuondolewa madarakani aliyekuwa rais wa taifa hilo Hosni Mubarak 2011. Katika vurugu hizo Wizara ya Afya ya Misri inasema watu 65 wameuwawa. Chama cha Udugu wa Kiislamu kinasema watu 61 wako mahututi huku vyanzo vingine vikisema zaidi ya watu 70 wameuwawa. Waziri wa Ulinzi wa Marekani Chuck Hagel amezungumza kwa njia ya simu na Mkuu wa Majeshi wa Misri, Abdel Fattah al-Sisi, ambae aliongoza mapinduzi ya Julai 3, ambae pia picha zake zimetapakaa katika mitaa ya Cairo. Nae Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Jonh Kerry amezungumza na viongozi wawili katika jeshi la Misri na kueleza kusikitishwa kwake na mkasa huo. Katika taarifa yake Kerry ametoa wito kwa mataifa ya Kiarabu kuchukua hatua za haraka kulikwamua taifa hilo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni