Jumamosi, 19 Oktoba 2013

Yanga yainyanyasa Simba

Mashabiki wa Simba na Yanga wakitambiana wakati wa maandamano maalumu yaliyofanywa kutangaza Nani Mtani Jembe inayoendeshwa na Kilimanjaro Premium Lager kwa mashabiki wa timu hizo jana, Dar es Salaam. 

Dar es Salaam. Saa chache kabla ya pambano, rekodi za miaka 48 iliyopita zinaonyesha Yanga imewafunga wapizani wake wa jadi, Simba magoli 112 dhidi ya 98 katika mapambano 97 waliyokutana tangu 1965 hadi sasa.
Simba na Yanga zitashuka kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kesho kukabiliana katika pambano la Ligi Kuu Tanzania Bara litakalopigwa kuanzia saa 10 jioni.
Gazeti hili lilifanya uchunguzi wake na kubaini kuwa kuanzia mwaka 1965 hadi mwaka huu,Yanga ina rekodi nzuri zaidi ya kucheka na nyavu tofauti na Simba.
Rekodi hizo zinaonyesha,katika kipindi hicho, Simba na Yanga zilikutana katika mashindano tofauti mara 97, ambapo Yanga ilipachika wavuni magoli 112 wakati Simba ilizamisha magoli 98.
Hata hivyo, katika kipindi hicho, Simba ndiyo inashikilia rekodi ya kushinda mabao mengi zaidi kupitia mechi moja baada ya kuitwanga Yanga mabao 6-0 katika pambano lililofanyika Julai 16,1977.
Katika pambano hilo mabao ya Simba yalikwamishwa wavuni na Abdalah Kibaden aliyefunga matatu dakika za 10, 42 na 89, Jumanne Hassan ‘Masimenti’ aliyefunga mawili dakika za 60 na 73 na lile la kujifunga la beki wa Yanga, Selemani Sanga dakika 20.
Pia, Kibaden ambaye sasa ni kocha wa Simba anajivunia rekodi binafsi ya kupachika mabao matatu kwenye mchezo mmoja ambayo hakuna aliyeivunja mpaka sasa.
Rekodi ya juu zaidi ya ushindi wa Yanga katika pambano dhidi ya Simba ni mabao 5-0 iliyoyapata katika pambano lililopigwa Juni mosi 1965 wakati huo Simba ikiitwa Sunderland.
Katika mchezo huo, Yanga ilijipatia mabao yake kupitia kwa Maulid Dilunga aliyefunga mawili dakika za 18 na 43, Salehe Zimbwe dakika 54 na 89 na Kitwana Manara dakika ya 86.
Lakini, mwaka jana Simba iliichabanga Yanga mabao 5-0 katika mechi ya mwisho ya Ligi Kuu Bara na mechi ya mwisho msimu uliopita ya ligi hiyo, Yanga ilishinda 2-0.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni