Jumamosi, 22 Juni 2013

Maskini CCM wanakumbuka shuka asubuhi?





Lauden Mwambona 

  • Hata mwenyekiti wake ambaye ndiye alikuwa Rais, hakuwa na ubavu wa kutamka mambo hadharani kabla ya kufikishwa kwenye Kamati Kuu na hatimaye Halmashauri Kuu.


Tangu CCM ifanye mabadiliko ya viongozi ngazi ya juu kwa kumteua Abdulrahman Kinana kuwa Katibu Mkuu imeonekana kurudi kwenye mstari wa utendaji kazi ulioanishwa kwenye nyaraka mbalimbali za chama.
Nyaraka za CCM ikiwamo Katiba zinatamka wazi kwamba jukumu lake kubwa ni kushika dola kwa kuunda Serikali. Zinasisitiza kwamba chama hicho kitaisimamia Serikali yake ili iweze kutenda haki na kutekeleza vyema ilani ya uchaguzi.
Ni kawaida kwa chama kinachounda Serikali  kinatakiwa kuwa na nguvu kuliko Serikali yenyewe.
Ni kwa msingi huo, CCM tangu enzi za Mwalimu Julius Nyerere ilikuwa ya kwanza  katika kujadili mambo muhimu ya kitaifa na kuweka msimamo imara kabla Serikali haijaanza kufanya lolote.
Hata mwenyekiti wake ambaye ndiye alikuwa Rais, hakuwa na ubavu wa kutamka mambo hadharani kabla ya kufikishwa kwenye Kamati Kuu na hatimaye Halmashauri Kuu. Enzi hizo, pamoja na kwamba walikuwapo viongozi ndani ya CCM au serikalini waliokuwa watoaji wa hoja za msingi, lakini CCM ilikuwa imara kuwaita mara moja na kuzijadili hoja zao kabla ya kutoa uamuzi.
Ndiyo maana kwa ngazi za mikoa na wilaya, wakuu wa mikoa na wilaya waliwajibika kutoa taarifa za kazi kwa Halmashauri ya CCM ngazi husika.
Viongozi wa CCM ngazi ya wilaya na mikoa walikuwa na nguvu kuliko wakuu wa mikoa  kwani enzi hizo chama kikiazimia kukuondoa mkuu wa idara kutokana na utendaji mbaya, ilikuwa ni mara moja unaondoka.
Hata hivyo baada ya kuingia mfumo wa vyama vingi, CCM ilianza kuyumba kiutendaji na kusababisha watendaji Serikali kushika hatamu. Tangu mwaka 1995 hadi mwaka jana, CCM ilishakubali Serikali iongoze chama badala ya yenyewe kuiongoza Serikali.
Vigogo wengi wa Serikali na wabunge walituhumiwa kwa wizi, rushwa, ufisadi wa kutisha, lakini CCM haikuchukua hatua zozote badala yake iliafikiana na Serikali yake watuhumiwa wote waendelee na kazi na ubunge.
Wapo walioshtakiwa mahakamani kuisababishia hasara Tanzania, lakini badala ya CCM kukaa vikao na kuwasimamisha  uanachama , iliogopa na kuwafanyia kampeni waendelee kuwa wabunge.
Wapo walioundiwa tume kwa ufisadi, badala ya CCM kukaa na kuwajadili kwa kina ili kutoa ufafanuzi mbele ya Watanzania, ilikaa kimya bila kauli yoyote. Mambo yalipozidi kipimo, ndipo mwaka jana CCM ilipoamua kuwarudisha kwenye uongozi wakongwe wa siasa na kutoa maelekezo kwamba CCM lazima iisimamie Serikali yake.
Maelekezo hayo yameanza kutekelezwa katika baadhi ya wilaya ambapo baadhi ya watendaji wameanza kuitwa na kuhojiwa kwa makosa mbalimbali.
Nao Watendaji wa CCM kitaifa  wakiongozwa na Kinana wamekuwa wakizunguka mikoa mbalimbali kufafanua utendaji wa kazi kati ya CCM na Serikali yake.
Wanasisiti za kwamba CCM lazima iisimamie Serikali yake kwa kuwaita kwenye vikao vya ndani watendaji wenye matatizo. Hatua hiyo inaanza kutekelezwa wakati watendaji wengi wa Serikali wameshajenga kiburi cha kwamba CCM haina nguvu kuliko Serikali.
Msimamo wa kutaka CCM iisimamie Serikali hauwatishi wakurugenzi wa halmashauri, watendaji wa idara ngazi za mikoa bali unawatisha wakuu wa mikoa  na wilaya pekee.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni