Syria imeutaka Umoja wa Mataifa kuchukua hatua kali dhidi ya
jinai zilizofanywa na makundi ya kigaidi yanayoungwa mkono na nchi za
kigeni nchini humo, kufuatia kuuliwa kwa umati na magaidi hao, watu
wasiopungua 123 huko katika mji wa Halab wa kaskazini mwa Syria. Shirika
la habari la Syria (SANA) limeripoti kuwa, magaidi wenye silaha walioko
nchini humo wameuwa watu wasiopungua 123 wengi wao wakiwa ni raia
katika shambulizi walilolifanya huko Khan Assal, magharibi mwa mji wa
Halab. Wizara ya Mambo ya Nje ya Syria imemuandikia barua tofauti
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na kuutaka umoja huo uzizuie nchi
zinazowaunga mkono magaidi hao baadhi yake zikiwa zinapakana na Syria,
ili magaidi hao wasiendelee kufanya mauaji ya umati dhidi ya raia nchini
humo. Barua hizo kwa Ban Ki Moon zimeeleza kuwa kundi hilo la magaidi
la huko Syria linalojiita kwa jina la Brigedi ya Ansar al Khalifa,
limekiri kuhusika na mauaji hayo ya Khan al Assal. Habari zinasema kuwa
baada ya kuwauwa raia hao wa Syria, magaidi hao walikata miili ya
wahanga na kuitupa katika shimo kubwa nje ya mji huo na pia kuichoma
moto baadhi ya miili ya watu waliowauwa. Wizara ya Mambo ya Nje ya Syria
pia imezikosoa vikali baadhi ya nchi kwa misimamo yao ya undumakuwili
kuhusiana na mapambano dhidi ya ugaidi. Barua hizo tafauti za Syria kwa
Umoja wa Mataifa pia zimeitaka taasisi hiyo kubwa ya kimataifa kuchukua
hatua za kweli za kupambana na ugaidi huko Syria.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni