Duru ya kwanza ya uchaguzi wa urais nchini Mali imefanyika leo
tarehe 28 Julai nchini humo. Viongozi wa nchi hiyo wametabiri kuwa,
karibu watu milioni saba wameshiriki kwenye uchaguzi wa leo. Katika duru
hiyo, wagombea 27 wamechuana vikali kuwania nafasi hiyo. Hii ni katika
hali ambayo Ibrahim Boubacar Keita, waziri mkuu wa zamani wa nchi hiyo
na Soumaila Cisse waziri wa zamani wa fedha, wanatajwa kuwa na nafasi
kubwa ya kuweza kushinda katika uchaguzi huo. Karibu askari 6300 wa
kulinda amani wa Umoja wa Mataifa wamechukua jukumu la kulinda usalama
katika uchaguzi huo. Zaidi ya hayo, askari 3200 wa Ufaransa pia bado
wako nchini humo, kwa kile kinachodaiwa ni kuvisaidia vikosi vya Umoja
wa Mataifa katika kazi zao za kulinda amani. Aidha chanzo kimoja cha
usalama nchini Mali kimetangaza habari ya kuweko askari wa kujitolea
wapatao 4500, ambao wameandaliwa na serikali ya Bamako kwa minajili ya
kudhaminia usalama katika zoezi zima la uchaguzi huo. Habari kutoka Mali
zimearifu kwamba, viongozi wengi wa nchi hiyo, wamepiga kura zao mjini
Bamako huku wengine wakipiga kura katika vituo rasmi vilivyosimamiwa na
polisi ya nchi hiyo. Hata hivyo pamoja na kuwepo askari wote hao, bado
kuna wasi wasi wa kutokea machafuko ya baada ya uchaguzi nchini humo.
Jana Harakati ya Umoja na Jihadi Magharibi mwa Afrika 'MUJAO', ilitoa
vitisho dhidi ya serikali ya Bamako na kuwataka wananchi kutokwenda
kupata kura. Aidha harakati hiyo, ilitishia kuwa, wapiganaji wake
watafanya mashambulizi dhidi ya vituo vya kupigia kura, hususan katika
maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo. Tangu wiki iliyopita, mji wa Kidal wa
kaskazini mwa Mali, umekuwa ukishuhudia machafuko yanayofanywa na
wapinzani ili kuvuruga hali ya usalama nchini humo. Kufichuliwa bomu la
kutengenezwa kienyeji karibu na soko la mji wa Kidal, kumezitia khofu
nyoyo za raia wa kawaiada kuhusiana na usalama wa eneo hilo. Aidha
utekaji nyara wa watu ni suala lingine lililozua khofu kubwa katika
uchaguzi wa leo. Wiki iliyopita, meya wa mji wa Kidal na mmoja wa
wafanyakazi wake, walitekwa nyara. Wapiganaji wa Harakati ya Kitaifa ya
Azawad waliisimamisha gari ya meya huyo, katika lango la kuingilia mji
huo na kuwateka nyara watu wawili kati ya wanne waliokuwamo ndani ya
gari hilo akiwemo meya huyo. Pamoja na hayo yote lakini weledi wa mambo
wanaamini kwamba, kufanyika uchaguzi wa leo, ni hatua moja mbele
kuelekea kwenye utawala mpya kikatiba nchini humo. Si vibaya kukumbusha
hapa kwamba, uchaguzi wa leo umefanyika ikiwa ni baada ya kupita miezi
sita, tangu Ufaransa ilipoingilia kijeshi mgogoro wa Mali. Aidha
uchaguzi wa leo umefanyika katika hali ambayo, zaidi ya watu 500,000
wanaishi kwenye kambi za wakimbizi wa ndani na inaaminika hawakupata
fursa ya kujiandikisha kama wapiga kura. Wakosoaji wanasema kuwa, jamii
ya kimataifa imeishinikiza Mali kufanya uchaguzi katika hali ambayo nchi
hiyo ilikuwa haijajiandaa kikamilifu kwa ajili ya zoezi hilo. Hata
hivyo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki moon amesema uchaguzi
ndiyo njia pekee ya kurudisha demokrasia katika nchi hiyo ya magharibi
mwa Afrika. Weledi wa mambo wanaamini kuwa, rais ajaye nchini Mali
atakuwa na majukumu makubwa na hatari, hasa kwa kuzingatia mgogoro na
vitisho vya wapinzani wa kaskazini mwa nchi hiyo, umasikini mkubwa na
kuzorota hali ya uchumi. Wakati huo huo, wachambuzi wengine wa mambo
wanaamini kuwa, uungaji mkono wa jamii ya kimataifa kwa serikali ya
Bamako na ahadi kemkem za kuipatia nchi hiyo msaada wa Euro bilioni
tatu, ni katika mambo yanayotia matumaini ya kutatuliwa mgogoro wa nchi
hiyo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni