Jumatatu, 12 Agosti 2013

Sheikh Ponda hospitalini chini ya ulinzi mkali


Habari kutoka Dar es Salaam zinasema kuwa, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda yupo chini ya ulinzi huku akitibiwa majeraha katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Sheikh Ponda alisafirishwa usiku wa manane kutoka Morogoro baada ya kupigwa risasi juzi alipokuwa akisindikizwa na wafuasi wake kwenda katika Msikiti wa Mungu Mmoja Dini Moja mara baada ya kumaliza kutoa mhadhara katika kongamano mjini hapo. Mwenyekiti wa Kongamano hilo, Sheikh Idd Mussa Msema, alidai kuwa Sheikh Ponda alipigwa risasi tatu begani na maafisa wa polisi waliokuwa wakijaribu kumkamata. Taarifa kutoka ndani ya familia ya Ponda zinasema kwamba baada ya kupata taarifa za kupigwa risasi, baadhi ya masheikh walifunga safari kwenda Morogoro na kumrejesha Dar es Salaam usiku huohuo. Kabla ya kurudishwa Dar es Salaam, imeelezwa kuwa Sheikh Ponda alipelekwa katika Zahanati ya Islamic Foundation kabla ya kusafirishwa hadi Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya kupatiwa matibabu. Polisi wanaendelea kushika doria Muhimbili huku ikitangazwa kuwa kiongozi huyo wa Waislamu ametiwa mbaroni na yuko chini ya ulinzi wa polisi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni